Baada ya kikao cha Kamati ya Taaluma kilichofanyika leo Mei 06, 2026, wajumbe wa kamati hiyo wakiongozwa na Mwenyekiti wa Kamati ya Taaluma, Profesa Francis Mwaijande, walifanya ziara katika eneo la ekari 40 lililopo Kampasi Kuu Dodoma kwa ajili ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa Jengo la Taaluma.
Katika ziara hiyo, wajumbe walipata fursa ya kuona hatua mbalimbali za utekelezaji wa mradi huo zinazotekelezwa kwa wakati mmoja ili kuhakikisha jengo hilo linakamilika na kuwa tayari kutumika ifikapo Juni 30, 2026.
Miongoni mwa shughuli zilizokaguliwa ni maendeleo ya ujenzi wa jengo hilo, uwekaji wa samani katika madarasa pamoja na upokeaji wa vifaa vya TEHAMA ikiwemo kompyuta kwa ajili ya matumizi ya kufundishia na kujifunzia.
Aidha, kamati ilijionea kuwa samani tayari zimefungwa katika madarasa matatu huku vifaa vya TEHAMA vikiendelea kuwasili sambamba na kazi za ukamilishaji wa maeneo ya nje ya jengo hilo.
Ziara hiyo imelenga kufuatilia maendeleo ya mradi huo muhimu unaotarajiwa kuongeza mazingira bora ya kujifunzia na kufundishia chuoni hapo.
Register Now